ILULA YETU

ILULA YETU
HOME: ILULA YETU BLOG

Jumatano, 8 Machi 2017

Rais Magufuli na mkewe wawasili mkoani Dodoma

Rais wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli, amewasili Mkoani Dodoma ambako pamoja na mambo mengine ataongoza Kikao cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa, Mkutano wa Halmashauri Kuu ya Taifa na Mkutano Mkuu Maalum wa Chama Cha Mapinduzi.

Mhe. Dkt. Magufuli ambaye ni Mwenyekiti wa CCM ataongoza kikao na mikutano hiyo kuanzia tarehe 10 - 12 Machi, 2017 Mjini Dodoma.

Mhe. Rais Magufuli akiwa na Mkewe Mama Janeth Magufuli waliwasili jana katika Ikulu ya Chamwino Mkoani Dodoma akitokea Mkoani Morogoro ambako jana tarehe 06 Machi, 2017 alizindua uwanja wa kisasa wa ndegevita wa Ngerengere.

SAA MBILI ZA MAANDAMANO WANAFUNZI BARIADI, Zilivyo simamisha mji wa Bariadi.

Wanafunzi wa shule ya sekondari Bariadi iliyoko katika halmashauri mjini wa Bariadi Mjini Bariadi wakiandamana katikati ya barabara kuu ya Bariadi-Lamadi, mjini Bariadi wakishinikizwa kurudishwa Mkuu wa shule yao ambaye alikuwa amepewa uhamisho Deus Toga, ambapo alikuwa amepelekwa shule ya sekondari Giriku na kuletewa Mkuu wa shule mwingine Paul Lutema ambaye walimkataa.


Mama Mlezi wa Rais Mstaafu Jakaya Kikwete Afariki Dunia

 

Mama mlezi wa aliyekuwa Rais Wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete, Bi Nuru binti Halfani Shomvi amefariki dunia katika Hospitali ya Muhimbili alipokuwa akitibiwa asubuhi ya leo.

Kupitia mtandao wa twitter, Rais Mstaafu Jakaya Kikwete akishukuru jamii kwa salamu za pole alizopokea amesema shughuli za msiba ziko nyumbani kwa marehemu Mzee Kikwete, Mtaa wa Caravan, Bagamoyo na maziko yatakuwa Bagamoyo mjini, kesho Jumatano Machi 8, 2017 saa 10 Alasiri.

"Mama amefariki jana usiku saa nane, akiwa na miaka 91. Baba yangu, Mzee Halfani Mrisho Kikwete alikuwa na wake wawili alipofariki 1998. Mama yangu mzazi Bi Asha binti Jakaya, aliyekuwa mke mkubwa wa Mzee Halfani Kikwete alifariki 1999; tukabaki na mama yetu huyu mdogo". Kauli ya Jakaya Kikwete

Naye Mbunge wa Chalinze Mhe. Ridhiwan Kikwete ambaye ni mjukuu wa marehemu ndiye aliyekuwa wa kwanza kuthibitisha kutokea kwa kifo hicho asubuhi ya leo.

"Ndugu na marafiki nasikitika kuwatangazia msiba/kifo cha Bibi yetu Bi. Nuru Khalfan Kikwete kilichotokea asubuhi hii katika Hospitali ya Muhimbili alipokuwa amelazwa kwa matibabu. Taratibu za mazishi tutajulishana" Amesema Ridhiwan Kikwete.
 
Ndugu wapendwa, nawashukuru sana kwa salamu za pole na upendo kufuatia kifo cha Mama yangu mdogo mpendwa Bi Nuru binti Halfani Shomvi. – JK
— Jakaya Kikwete (@jmkikwete) March 7, 2017




CUF ya Maalim Seif kuiburuza CUF ya Prof.Lipumba mahakamani

Bodi ya Wadhamini ya Chama cha Wananchi (CUF ), imefungua kesi ya madai dhidi ya wanachama wake nane akiwemo Naibu Katibu Mkuu, Magdalena Sakaya

Kesi hiyo imefunguliwa leo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu ikitaka wanachama hao wasijihusishe na harakati  zozote za chama hicho.

Mbali ya Sakaya ambaye pia ni mbunge wa Kaliua mkoani Tabora, wadaiwa wengine ni Thomas Malima, mbunge wa Mtwara Mjini,Mafta Nachumu, Omar Mhina Masoud, Abdul Kambaya, Salama Masoud, Zainabu Mndolwa na Jafari Mneke.

Maombi hayo mbayo yametajwa mbele ya Hakimu Mkazi, Wilbard Mashauri yamewasilishwa na Wakili wa bodi, Hashim Mziray na yamepangwa kusikilizwa kesho.

Katika maombi hayo yaliyopewa namba 1 ya mwaka 2017, bodi inaiomba mahakama kutoa zuio kwa wadaiwa kutojihusisha katika masuala yeyote yanayohusiana na chama hicho.

Mbali ya maombi hayo, pia Wakili Mziray amewasilisha maombi madogo ya kuiomba mahakama kuwaamuru wadaiwa wasijihusishe na mikutano ya chama hicho.
 
Aidha, Mziray aliomba maombi yao madogo yasikilizwe kwa upande mmoja wa wadai tu kwa kuwa wamechelewa kuwapatia nyaraka za madai yao wadaiwa.

"Mheshimiwa tunaomba tusikilizwe upande mmoja ukizingatia maombi yameletwa chini ya hati ya dharula na kwa mujibu wa sheria mahakama hii... inayo mamlaka ya kufanya hivyo".

Hakimu Mashauri alisema anakubaliana na upande wa wadai na maombi hayo yatasikilizwa kesho mahakamani hapo.

Hatua ya Bodi ya CUF, kukimbilia mahakamani inakuja ikiwa ni siku moja baada ya upande unaomuunga mkono Katibu Mkuu wa chama hicho, Maalim Seif Shariff Hammad kupinga uteuzi wa Mwenyekiti wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba.

Uteuzi wa Profesa Lipumba ambao unapingwa ni ule alioufanya Machi 6, mwaka huu baada kuwaondoa katika nafasi zao, Mkurugenzi wa Mipango na Uchaguzi, Omar Ali Shehe.

Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma, Salim Abdull Bimani, Mkurugenzi wa Fedha na Uchumi, Abdullah Bakar Hassan.

Wengine ni Pavu Juma, Naibu Mkurugenzi wa Haki za Binadam na Sheria, Mahmoud Ali Mahindo na Katibu wa Jumuiya ya Vijana, Yusuph Salim.